JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA 
WIZARA YA UJENZI NA UCHUKUZI 
MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA 


TAARIFA KWA UMMA UFAFANUZI KUHUSIANA NA EL NIÑO 

Dar es Salaam, 03 Mei, 2023: 
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inapenda kutoa ufafanuzi juu ya uwepo wa hali ya El Niño na uhusiano wake katika mienendo ya mvua nchini. El Niño ni mfumo wa hali ya hewa unaosababishwa na uwepo wa joto la bahari la juu ya wastani katika eneo la kati la kitropiki la bahari ya Pasifiki. 

Hali hii kwa kawaida huambatana na vipindi vya mvua kubwa vinavyoweza kusababisha mafuriko. Mamlaka ya Hali ya Hewa, ilifuatilia mifumo ya hali ya hewa wakati wa maandalizi ya msimu wa mvua za Masika (Machi hadi Mei), 2023 na inaendelea kufuatilia mifumo hiyo ikiwemo El Niño.

Aidha, kama ilivyoanishwa kwenye taarifa ya utabiri wa msimu wa mvua za Masika iliyotolewa terehe 22 Februari, 2023 viashiria hivyo vilikuwa vinaonesha mvua hizi kuanza mwezi Machi, katika maeneo mengi na kuisha katika wiki ya nne ya mwezi Mei 2023 katika maeneo mengi ingawa mwendelezo wa mvua za nje ya msimu ulitarajiwa mwezi Juni 2023 katika maeneo machache. Maandalizi ya Utabiri wa msimu wa Kipupwe (Juni hadi Agosti, 2023) unaendelea na taarifa yake inatarajiwa kutolewa mwishoni mwa mwezi Mei. 

Kwa taarifa hii wananchi wanashauriwa kuendelea kuzingatia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania sambamba na kutafuta, kupata na kuzingatia ushauri wa wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazotokana na hali mbaya ya hewa. 

Imetolewa na: Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania